
MAHAKAMA YAMPA USHINDI MPINA DHIDI YA INEC
- Habari
- September 11, 2025
- No Comment
- 26
Mahakama Kuu, Masjala Kuu Dodoma, imetoa uamuzi kumruhusu mwanachama wa ACT-Wazalendo, Luhaga Mpina, kuendelea na mchakato wa kurejesha fomu ya kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mahakama imeeleza kuwa zuio lililowekwa na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) dhidi ya Mpina, ambalo lilimzuia kurejesha fomu na kumnyima haki ya kusikilizwa, lilikuwa kinyume cha sheria na Katiba ya nchi.
Uamuzi huo umetolewa Septemba 11, 2025, katika shauri Na. 21692/2025 lililofunguliwa na Bodi ya Wadhamini wa ACT-Wazalendo pamoja na Luhaga Mpina dhidi ya INEC na Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Mahakama imebainisha kuwa uamuzi wa INEC uliofanyika Agosti 27, 2025, uliathiri haki za walalamikaji, na hivyo walipewa fursa ya kurejesha fomu haraka ili kuendelea na mchakato wa kugombea urais.
Hata hivyo, Mahakama imekataa ombi la walalamikaji la kutaka kulipwa fidia ya shilingi milioni 100. Uamuzi huu ulisomwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Abdi Kagomba.