
MAKUSANYO YA GST YAONGEZEKA KWA ASILIMIA 91
- Habari
- March 27, 2025
- No Comment
- 70
Makusanyo ya ndani ya Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) yameongezeka kutoka wastani wa shilingi 1,251,428,472.91 mwaka 2021 hadi shilingi 2,394,211,348 mwaka 2023/2024, sawa na ongezeko la asilimia 91.32.
Hayo yamesemwa na Kaimu Mtendaji Mkuu wa Taasisi hiyo Notze Banteze wakati akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu mafanikio na mwelekeo wa GST ndani ya uongozi wa Serikali ya awamu ya sita, katika ukumbi wa idara ya Habari na Maelezo Jijini Dodoma.
Banteze amesema bajeti ya taasisi hiyo pia imeongezeka kutoka wastani wa shilingi bilioni 10 mwaka 2021/2022 hadi bilioni 110 mwaka 2024/2025 sawa na ongezeko la asilimia 1,000 kwa ajili ya kukamilisha majukumu mbalimbali ya taasisi ikiwemo miradi ya maendeleo.
Aidha, Banteze ameongeza kuwa GST imekamilisha utoaji wa mafunzo kwa wachimbaji wadogo wa madini 2,733 kuhusu uchukuaji wa sampuli wakilishi na utambuzi wa jiolojia ya maeneo yenye uwepo wa madini. Mafunzo yalifanyika katika mikoa ya Lindi, Morogoro, Geita na Mwanza.