
WANANCHI WAASWA KUHAKIKI KIASI CHA GESI WANACHONUNUA
- Habari
- March 25, 2025
- No Comment
- 81
Katika kuunga mkono kampeni ya matumizi ya nishati safi ya kupikia ambayo kinara wake ni Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wakala wa Vipimo nchini (WMA) inendelea kufanya ukaguzi na uhakiki wa vipimo kwenye mitungi ya gesi ili kuhakikisha kuwa wanunuzi wa gesi wanapata kiasi sahihi kulingana na thamani ya fedha wanayolipa kwa ajili ya huduma hiyo.
Hayo yamesemwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo (WMA) Alban Kihula wakati akielezea mafanikio ya WMA katika kipindi cha miaka minne ya serikali ya Awamu ya sita, jijini Dodoma na kuongeza kuwa Mwananchi anapaswa kufahamu ni gesi kiasi gani amenunua kwaajili ya matumizi yake.
Kihula amesema katika eneo hili, Sheria ya Vipimo Sura 340 inawataka wauzaji wote wa mitungi ya gesi kuwa na mizani zilizohakikiwa na Wakala wa Vipimo, ili mnunuzi ajiridhishe na uzito wa gesi anayonunua.
Aidha, Kihula ametoa rai kwa wauzaji wote wa gesi nchini, kuhakikisha wanatumia mizani zilizohakikiwa na WMA kwenye biashara ya gesi, lakini pia amewataka wanunuzi wa Nishati hiyo (Wananchi) kuhakikisha kiasi cha gesi wanachopokea kwenye mitungi kupitia Mizani hiyo iliyohakikiwa na Wakala wa Vipimo.