
COSOTA KUWASAKA WEZI WA KAZI ZA WASANII
- Habari
- March 21, 2025
- No Comment
- 74
Ofisi ya Haki Miliki Tanzania (COSOTA) imesema itaendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi kufanya misako katika maeneo yote nchini ili kupambana na Uharamia wa mtandao na kuhakikisha ulinzi na usalama wa kazi za Wasanii nchini.
Kauli hiyo imetolewa na Afisa mtendaji mkuu na Msimamizi wa COSOTA Doreen Sinare, katika Mkutano na Waandishi wa Habari uliofanyika leo Machi 21, Idara ya Habari na Maelezo Jijini Dodoma na kuongeza kuwa lengo la kufanya misako hiyo ni kuhakikisha wasanii wananufaika na kazi zao.
Doreen amesema mpaka hivi sasa Operesheni hiyo imefanyika katika mikoa ya mikoa ya Dar es Salaam, Kagera, Dodoma, Tabora, Shinyanga, Songwe, Mwanza, Morogoro, Arusha, Kilimanjaro, Lindi, Mtwara, Manyara na Mara ikiwa ni utekelezaji wa Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki ya mwaka 1999, kanuni ya uzalishaji na usambazaji ya Mwaka 2006 na kanuni ya Ufifilishaji wa makosa ya Hakimiliki ya mwaka 2020.
Katika hatua nyingine COSOTA imekusanya migogoro 136 ya Wasanii kuhusu haki Miliki, katika kipindi cha miaka minne ya utawala wa awamu ya sita huku migogoro 118 ikifanyiwa kazi na kutolewa majibu, migogoro nane ikiwa bado inaendelea kusikilizwa na migogoro 10 kati ya hiyo haikumalizika kutokana na wahusika kushindwa kufika kwenye mamlaka hiyo.